Ebrahim Raisi amesema hayo katika hotuba yake kwenye mkutano wa 77 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mjini New York na kueleza kwamba, hamu na shauku ya kutaka kuweko uadilifu kama ni adia ya Mwenyezi Mungu iko katika dhamira za wanadamu wote
Rais wa Iran amesisitiza katika hotuba yake hiyo kwamba, Jamhuri ya Kiiislamu ya Iran inaunga mkono kuweko dunia yenye uadilifu, kwani uadilifu unaleta umoja na kwamba, dhulma inachochea na kuleta vita na machafuko.
Rais wa Iran amesema katika sehemu nyingine ya hotuba yake hiyo kwamba, Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran yalikuwa ni harakati ya wananchi wa Iran kuelekea ukweli na uhakika, ambapo licha ya kuweko fitina mbalimbali lakini yaliweza kulinda utukufu wa malengo yake.
Kuhusiana na makubaliano ya nyuklia ya JCPOA, Rais Ebrahim Raisi amesema kuwa, Marekani ''ilikanyaga'' na kukiuka makubaliano hayo ya kimataifa yaliyosainiwa mwaka 2015, na kuongeza kuwa Iran haina nia ya kutengeneza silaha za atomiki kama ambavyo amesisitiza azma ya Tehran ya kuwa na uhusiano mwema na majirani zake wote.
Katika sehemu nyingine ya hotuba yake, Rais Ebrahim Raisi amesema kuwa, Iran ni mhanga wa ugaidi na amelitaka Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kufuatilia jinai ya kigaidi ya kuuawa shahidi Luteni Jenerali Qassem Soleimani, aliyekuwa Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (SEPAH) ambaye aliuawa katika shambulio la anga la Marekani Januari 3, 2020 huko Baghdad Iraq.
/342